SIONI TATIZO KLABU KUMILIKIWA NA MTU MMOJA,MFUMO HUU UNAWEZA KUBADILISHA TASWIRA YA SOKA LA TANZANIA

SIONI TATIZO KLABU KUMILIKIWA NA MTU MMOJA,MFUMO HUU UNAWEZA KUBADILISHA TASWIRA YA SOKA LA TANZANIA

Like
240
0
Tuesday, 10 November 2015
Slider
Na Omary Katanga
Mfumo wa vilabu vinavyotajwa kuwa ni vikubwa nchini,Simba na Yanga,wa kuwa na wanachama wenye kutoa maamuzi yanayohusu klabu zao,ni wazi kuwa umepitwa na wakati kwa karne hii ya sasa katika soka lenye ushindani duniani.
Mfumo huu umekuwa ukiwapa nguvu wanachama ya kufanya kile wanachotaka kwakuwa katiba za vilabu vyao vinawatambua,na ndiyo maana wakati mwingine wamekuwa wakishinikiza uongozi kufanya maamuzi yasiyofaa kwakuwa tu wanayohaki y kuamua.
Ukiangalia utaratibu uliopo kwa vilabu vya bara la ulaya na maeneo mengi ya afrika,huwezi kukuta mfumo huu wa wanachama kuwa na nguvu ya maamuzi na badala yake kunakuwepo na mmiliki mmoja anayemiliki hisa nyingi zinazompa mamlaka ya kufanya maamuzi ya mwisho.
Kwa wakati tulionao sasa ipo haja ya vilabu vya tanzania navyo vikaingia katika mfumo wa kumilikiwa na watu wafanyabiashara binafsi ili kurahisisha maendeleo ya soka katika nchi yetu,kitendo kitakachopunguza hata vurugu zisizokuwa za lazima ambazo mara nyingi zimekuwa zikiripotiwa kufanywa na wanachama.
Lazima tukubali bila kusita kwamba klabu inapomilikiwa na mtu mmoja inakuwa na mabadiliko makubwa katika maendeleo ya soka na ndiyo maana ukijaribu kumuuliza mtu yeyote anayejua nini maana ya uwekezaji katika vilabu,nina uhakika kwamba  atakujibu bila kusita kwamba  hilo ni jambo lenye manufaa sana kwa wakati huu.
Hebu tuangalie mfano huu,ambapo wiki chache tu zilizopita mfanyabiashara mkubwa na maarufu hapa nchini,Mohamed Dewji, aliweka wazi dhamira yake ya kutaka kuinunua klabu ya Simba na kuwekeza bilioni 20 kwa ajili ya kumiliki klabu hiyo, kwa kile alichodai kwamba lengo lake ni kuifanya klabu hiyo itishe kisoka ndani na nje ya nchi.
Katika dili hilo Dewji anataka kumiliki hisa za klabu ya Simba kwa asilimia 51,na asilimia nyingine zinazobaki zitamilikiwa na watu wengine wenye uwezo kununua hisa hizo wakiwemo wanachama pia watakaopenda kufanya hivyo.
Kama Dewji atafanikiwa katika mpango huo,atakuwa mfanyabiashara wa kwanza kuleta mabadiliko ya mfumo wa maamuzi kwenye klabu ya Simba,yenye historia kubwa katika medani ya soka la tanzania,na kuifanya klabu hiyo kuingia katika mfumo wa kibiashara utakaowezesha kutanua wigo kandanda katika klabu hiyo ya Msimbazi.
Hivi karibuni nilifanya mazungumzo na aliyekuwa mwenyekiti wa klabu ya Simba,Ismail Aden Rage kutaka kujua maoni yake juu ya mpango wa Dewji kutaka kuichukua klabu,akanijibu kuwa hili jambo linahitaji utulivu wa hali ya juu katika kulifanyia maamuzi,na akasisitiza kuwa ni lazima jambo hilo likapelekwa kwanza kwa wanachama.
Kwa hali hiyo unaweza kukubaliana na mimi kwamba nguvu waliyonayo wanachama katika kufanya maamuzi ndani ya klabu ni kubwa kuliko waliyonayo viongozi wao,na hasa ukizingatia kuwa wamewekwa madarakani kwa nguvu ya kura za wanachama hao hao.
Mwisho.

Comments are closed.