Kenyatta amekuwa gumzo kuu katika mitandao ya kijamii nchini Kenya wakati akitarajiwa kulihotubia taifa leo.

Kenyatta amekuwa gumzo kuu katika mitandao ya kijamii nchini Kenya wakati akitarajiwa kulihotubia taifa leo.

Like
566
0
Thursday, 04 April 2019
Global News

Uhuru Kenyatta amekuwa gumzo kuu katika mitandao ya kijamii nchini Kenya wakati akitarajiwa kulihotubia taifa leo.

 

Kiongozi huyo mkuu nchini Kenya anatarajiwa kuizungumzia hali ya mambo nchini katika hotuba anayotarajiwa kuitoa bungeni leo mchana.

Na hili linatarajiwa kufanyika wakati ufisadi, deni kubwa la taifa na suala la ukosefu wa ajira na mishahara yakizungumziwa pakubwa na wakenya ambao wametumia fursa kumshinikiza kiongozi huyo kuyazungumzia leo.

Swali kuu ni je, Rais Uhuru Kenyatta atasema nini leo kipya katika hotuba yake ya taifa?

Baadhi ya Wakenya wanauliza, ‘Ni kipi kipya atakachotuambia ambacho hatujakisikia?’

Baadhi wamegusia kwamba wangependa sana rais Kenyatta aangazie kuhusu matumizi ya fedha serikalini na uhaba wake unaochangia kuongezeka kwa mikopo – jambo linalowatia wasiwasi raia wengi.

Uchumi wa Kenya umekuwa ukikua kwa kiwango cha wastani kila mwaka tangu kiongozi huyo aingie madarakani, lakini baadhi ya Wakenya wanasema hawajahisi manufaa ya ukuaji huo.

Serikali imeshutumiwa kuchukua mikopo kwa wingi, baadhi wakikadiria kwamba serikali hiyo imepitisha viwango vya ukopaji vya serikali zote za awali tangu uhuru.

Mchambuzi wa kisiasa nchini Kenya na Mhadhiri, katika Chuo Kikuu cha Nairobi Hezron Mogambi anahoji, swali ambalo limekuwa likiibuka miaka ya hivi karibuni ni iwapo Kenya itaweza kujimudu kulipa madeni ambayo yamekuwa yakijilimbikiza.

Wakopaji wa kimataifa kupitia shirika la Moody’s katika siku za nyuma wameishusha Kenya daraja katika masuala ya ukopaji.

Sababu zilizotolewa kwa hatua hiyo ni pamoja na hali ya kiuchimi isiyoonyesha matumaini kutokana na kulimbikizwa kwa madeni, kutegemea sana madeni ya kibishara na mahitaji ya kifedha mengi katika uchumi wa Kenya kutokana na miradi.

‘Hali hii ambayo inaonyesha ishara ya Kenya kutoweza kuyalipa madeni, ni suala linalotatiza na kuzua changamoto kwa serikali na wananchi kwa jumla,’ anasema Mogambi katika makala aliyoiandika kwenye BBC Swahili.

Bw Kenyatta, hata hivyo amekuwa akisema kuwa uwekezaji wa pesa hizo katika miradi ya miundo mbinu, mfano reli ya kisasa kutoka Mombasa hadi Nairobi iliyogharimu $3.2bn (£2.5bn), itasisimua ukuaji wa uchumi nchini.

Jambo jingine ambalo baadhi ya wakenya katika mitandao ya kijamii waliloinuka nalo moyoni na wanalotaka hatua madhubuti kuchukuliwa kulihusu ni ufisadi.

Limekuwa donda sugu kwa miaka kadhaa nchini.

Wakenya wanataka rais atoe muongozo au muelekeo thabiti katika kukabiliana na matatizo ya kiuchumi.

Kumekuwa na kilio cha umma nchini Kenya kufuatia kashfa mbali mbali za rushwa ambazo hazijatatuliwa.

Baadhi wamekuwa wakieleza kwamba wanahisi Rais hajachukua hatua stahiki na kwa muda mrefu kufikia sasa amewaendekeza ‘wahalifu’ katika serikali.

Rais Kenyatta amekuwa akisema juhudi zake za kukabiliana na ufisadi zimehujumiwa na idara mbali mbali.

Mwaka 2015, Kenyatta aliwasimamisha kazi na kisha akawafuta mawaziri watano na maafisa wengine wa ngazi ya juu serikali waliotuhumiwa kujihusisha katika ufisadi.

Waziri mwingine alijiuzulu kutokana na shinikizo la umma.

Katika orodha ya mataifa yanayoshuhudia ufisadi Kenya ipo katika nafasi ya 144 chini ya mataifa 180 kwa mujibu wa utafiti wa shirika la kimataifa la Transaparency International mnamo 2018.

Kwa miaka mingi, kumekuwa na wito wa kwamba ufisadi unastahili kutangazwa janga la kitaifa nchini Kenya.

Shinikizo limeongezeka kwa rais Uhuru Kenyatta asiteteleke katika vita dhidi ya ufisadi.

Raia wanamtaka kiongozi huyo pia aidhinishe hatua zitakazohakikisha kwamba vita hivyo vinaendelezwa hata kwa uongozi ujao na wahalifu wachukuliwe hatua za kisheria.

Kimsingi wanashinikiza kwamba vitendo vidhihirike zaidi ya maneno ‘matupu’.

Kuna waliochukua fursa hii kumsifia rais kwa jitihada zake katika kuimarisha nchi na kufikia malengo manne makuu aliyoahidi katika kampeni ya kuchaguliwa kwake uongozini.

Ajenda hizo kuu ambazo kiongozi wa Kenya ametilia maanani ni pamoja na kuimarisha sekta ya viwanda, afya, makaazi kwa bei nafuu na chakula.

Tayari Hazina ya kitaifa ya matibabu nchini Kenya (National Hospital Insurance Fund) imeshaanza kutekeleza afya kwa umma.

Lakini pia kuna wanaopigia upatu sekta ya usalama kwa mahali ambapo taifa limefika kwa sasa.

Ijapo ni suala linalojadiliwa, kuna wanaosifia hatua angalau ndogo katika sekta hiyo.

Kwa mfano wa hivi karibuni, muitikio ulioshuhudiwa katika shambulio lililotekelezwa na wapiganaji wenye itikadi kali za dini ya kiislamu jijini Nairobi tarehe 15 Januari umeonekana kama mapinduzi makubwa ya Propaganda kwa upande wa wapiganaji hao na kudhihirisha uwezo wa Kenya kukabiliana na ugaidi.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *