Korea kaskazini yasusia mazungumzo ya amani na Korea kusini kuhusu mazoezi ya vita

Korea kaskazini yasusia mazungumzo ya amani na Korea kusini kuhusu mazoezi ya vita

2
1350
0
Friday, 16 August 2019
Global News

Korea kaskazini imepinga mazungmzo ya ziada ya Korea kusini, na kusema uamuzi huo ni “makosa ya hatua za Korea kusini”.

Imetoa taarifa kufuatia hotuba ya rais wa Korea kusini Moon Jae-in hapo jana Alhamisi.

Wakati huo huo, mapema leo Ijumaa Korea kaskazini imefyetua makombora mawili baharini kutoka pwani ya mashariki, jeshi la Korea kusini limearifu.

Likiwa ni jaribio la sita la aina hiyo, na linafanyika chini ya mwezi mmoja.

Makombora hayo mawili “ambayo hayakutambuliwa ” yalifyetuliwa mwendo wa saa mbili asubuhi Alhamisi na kusafiri umbali wa kilomita 230 kufika ujuu wa 30km, Afisa wa vikosi jumla Korea kusini amesema.

Msururu wa majaribio hayo yanajiri baada ya rais wa Marekani Donald Trump na mwenzake wa Korea kaskazini Kim Jong-un kukubaliana katika mkutano mnamo Juni kuanza upya majadiliano ya jitihada za kusitisha matumizi ya silaha za nyuklia.

Korea kaskazini imekabiliwa na vikwazo vya kimataifa kwa kutengeneza silaha za nyuklia.

Korea kusini imesema nini?

Katika hotuba hiyo, ya kuadhimisha uhuru wa Korea dhidi ya utawala wa Japan, rais Moon aliapa kuiunganisha rasi ya Korea kufikia mwaka 2045.

Korea iligawanyika na kuwa mataifa mawili mwishoni mwa vita vya pili vya dunia.

Rais Moon amesema lengo la kufanikiwa kuacha matumizi ya silaha za nyuklia katika rasi ya Korea ni jambo muhimu zaidi wakati mazungumzo kati ya Kaskazini na Kusini yakionekana kukwama.

“Rasi mpya ya Korea, ambayo italeta amani na ustawi kwayo, na mashariki mwa Asia, pamoja na katika dunia nzima, inatusubiri,” alisema katika hotuba hiyo aliyoitoa kwenye televisheni.

Korea kaskazini imelipokea vipi?

Katika taarifa yake, Korea kaskazini imehoji maana ya mazungumzo wakati “hata katika wakati huu Korea Kusini inaendeleea kufanya mazoezi ya kijeshi ya pamoja na kuzungumzia suala la uchumi wa amani na utawala wa amani. Haina haki ya kufanya hivyo.”

Katika linaloonekana kuwa ni shambulio dhidi ya rais Moon, taarifa hiyo imeendelea kusema “Tunajiuliza pia iwapo yupo timamu katika fikra zake wakati anapotaja ‘mazungumzo’ baina ya Kaskazini na Kusini wakati anaendeleza taswira ya vita inayopanga kuangamiza vikosi vyetu katika siku 90.

“Ni mwanamume aliyekosa haya.”

Korea kaskazini imekasirishwa na mazoezi ya kijeshi baina ya Korea kusini na Marekani , ikieleza kuwa yanakiuka makubaliano yaliofikiwa baina ya rais Donald Trump na rais Moon.

Imewahi kuyataja mazoezi hayo kuwa “mazoezi ya vita”.

Katika barua ya hivi karibuni kwa Trump, kiongozi wa Korea kaskazini Kim Jong-un anaarifiwa kuwa alilalamika “kuhusu gharama kubwa na kichekesho” cha mazoezi hayo.

Mkwamo uliopo katika mazunguzo ya kuistisha matumizi ya silaha za nyuklia ni makosa ya uamuzi wa Korea kusini kufanya mazoezi ya kijeshi, msemaji wa utengamano kutoka Korea kaskazini amesema.

“Hatuna maneno ya ziada kuzungumza na maafisa wa Korea kusini,” afisa huyo amesema katika taarifa iliyopeperushwa kwenye televisheni ya taifa ya Korean Central News Agency.

cc;BBCswahili

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *