Mtoto wa kiume wa Bin Laden ”amefariki”

Mtoto wa kiume wa Bin Laden ”amefariki”

Like
671
0
Thursday, 01 August 2019
Global News

Mwana wa kiume wa muasisi wa al-Qaeda Osama Bin Laden, Hamza,amefariki , kwa mujibu wa maafisa wa ujasusi wa Marekani.

Taarifa kuhusu mahala au tarehe ya kifo cha Hamza Bin Laden bado haijawa wazi katika ripoti ya chanzo hicho cha habari.

Mwezi Februari, Serikali ya Marekani iliahidi kutoa dola milioni 1 kwa ajili ya yeyote atakayetoa taarifa zitakazosaidia kutambua ni wapi alipo.

Hamza Bin Laden, anayedhaniwa kuwa na umri wa miaka 30, alikuwa ametoa ujumbe mbalimbali wa sauti na video akitoa wito wa kufanya mashambulio dhidi ya Marekani na nchi nyingine.

Ripoti zilitolewa kwanza na mashirika ya habari ya NBC na New York Times.

Hamza Bin Laden aliwatolea wito wapiganaji wa jihadi kulipiza kisasi mauaji ya baba yake aliyeuliwa na kikosi maalum cha Marekani nchini Pakistan mnamo mwezi Mei 2011.

Kadhalika alikuwa amewatolea wito watu wa rasi ya Arabia kulipiza kisasi. Saudi Arabia ilimyang’anya uraia mwezi Machi.

Aliaminika kuwa katika kifungo cha nyumbani nchini Iran lakini ripoti nyingine zilisema kuwa huenda alikuwa akiishi katika mataifa ya Afghanistan, Pakistan na Syria.

Wizara ya mambo ya nje ya Marekani ilisema kuwa nyaraka zilizokamatwa katika uvamizi wa mwaka 2011 katika nyumba ya baba yake ya Abbottabad, Pakistan, zinaonyesha kuwa Hamza Bin Laden alikuwa anaandaliwa kuchukua utawala wa al-Qaeda.

Vikosi vya Marekani pia viliripotiwa kubaini video hii ya harusi yake akimuoa binti wa afisa mwingine wa ngazi ya juu wa al-Qaeda ambayo ilidhaniwa kufanyika nchini Iran

Baba mkwe wake alikuwa ni Abdullah Ahmed Abdullah au Abu Muhammad al-Masri, ambaye anatafutwa kwa madai ya kuhusika katika mashambulio ya ugaidi ya mwaka 1998 dhidi ya balozi za Tanzania na Kenya.

Al-Qaeda lilikuwa ni kundi lililotekeleza mashambulio mabaya ya ugaidi ya Septemba 11, 2001 dhidi ya Marekani, lakini hadhi yake kwa sasa imeshuka katika kipindi cha miongo kadhaa iliyopita baada ya kuibuka kwa umaarufu wa kundi la Islamic State.

Ni ishara ya jinsi taarifa chache kumuhusu Hamza Bin Laden kiasi kwamba maafisa hawakuweza kuthibitisha umri wake.

Katika miezi ya hivi karibuni walisema kuwa huenda alikuwa nchini Afghanistan, Pakistan au Iran. lakini hawakuweza hata kusema ukweli hasa ni nchi gani mmoja wa watu ambao Marekani ”inawatafuta sana” anaishi.

Zawadi ya dola milioni moja kwa yeyote atakayetoa taarifa kumuhusu ilikuwa ni hatua si tu ya uwezekano wa hatari anayoweza kusababisha lakini pia ilikuwa ni ishara ya umuhimu kwa al-Qaeda na propaganda yao.

Hamza alikuwa ni mtoto pekee aliyekuwepo wakati baba yake aliposaidia kupanga njama za mashambulio ya Septemba 11 lakini, kwa mujibu wa wakuu wa kundi hilo lenye itikadi kali, alikuwa pamoja naye wakati wa mashambulio hayo.

Kwa mtoto wa kiume ambaye alikuwa akifundishwa kuichukia Marekani, kukwepa mauaji ya ulipizaji kisasi mikononi mwa kikosi maalumu lingekuwa ni jambo ambalo lingesalia akilini mwa watu.

Katika miaka ya hivi karibuni alituma ujumbe mtandaoni akitoa wito kwa mashambulio dhidi ya Marekani na washirika wake.

Al-Qaeda: Taarifa muhimu

  • Alifahamika nchini Afghanistan katika miaka ya mwisho ya 1980, kama mwarabu aliyejitolea kujiunga na kikosi cha Afghanstan kilichoungwa mkono na mujahideen kilichopigana kuvifukuza vikosi vilivyoteka eneo la Usovieti
  • Osama Bin Laden alianzisha shirika la kusaidia wahudumu wa kujitolea ambalo lilikuja kutambuliwa kama al-Qaeda, au “ngome”
  • Aliondoka Afghanistan mnamo mwaka 1989, na kurejea tena mwaka 1996 kuongoza makambi ya mafunzo ya kijeshi ya maelfu ya waislamu kutoka mataifa ya kigeni.
  • Al-Qaeda ilitangaza “vita vitakatifu ” dhidi ya Wamarekani,wayahudi na washirika wao.

cc;BBCswahili

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *