Rajoelina atangazwa mshindi uchaguzi wa Madagascar

Rajoelina atangazwa mshindi uchaguzi wa Madagascar

Like
607
0
Friday, 28 December 2018
Global News

Kiongozi wa zamani wa Madagascar Andry Rajoelina ametangazwa mshindi wa uchaguzi wa rais wa taifa hilo la kisiwa cha bahari ya Hindi katika matokeo ya awali yaliotangazwa na tume ya uchaguzi Alhamisi.

Rajoelina alikuwepo wakati tume ya uchaguzi ikitangaza kwamba amepata asilimia 55.66 ya kura, ikilinganishwa na asilimia 44.34 ya mshindani wake Marc Ravalomanana – ambaye hakuwepo wakati wa kutangazwa matokeo.

Ravalomanana, ambaye pia ni rais wa zamani, amekosoa uchaguzi katika kisiwa hicho kilichoko nje ya pwani ya Afrika kwa kile alichokiita udanganyifu mkubwa. Mahakama ya katiba hivi sasa ina muda wa siku tisa kutangaza matokeo ya mwisho.

Siasa nchini Madagascar, ambayo ni koloni la zamani la Ufaransa na mojawapo ya mataifa maskini zaidi duniani, kwa muda mrefu zimekuwa zikizongwa na mapinduzi ya mara kwa mara na machafuko. Rajoelina na Ravalomamana wana historia ya uhusiano mgumu kati yao, baada ya Rajoelina kuchukuwa nafasi ya Ravalomana kama akiongozi wa taifa kufuatia mapindizi ya kijeshi mwaka 2009.

Duru ya kwanza ya kura katika uchaguzi huu wa karibuni ilifanyika mwezi Novemba, ambapo Rajoelina alishinda kwa asilimia 39 dhidi ya asilimia 35 ya Ravalomanana. Duru ya pili ilifanyika mapema mwezi huu. Ravalomanana alielezea wasiwasi kuhusu kile ambacho chama chake kilisema vilikuwa vitambulisho bandia vya kupigia kura.

Historia ya migogoro

Madagascar imepitia mgogoro wa muda mrefu mapema mwaka huu baada ya bunge kupitisha sheria mpya ambayo upinzani ulisema itaipendelea serikali iliyoko madarakani.

Kwa zaidi ya mwezi mmoja, wabunge kadhaa wa upinzani na wafuasi wao walikusanyika kila siku katikati mwa mji mkuu wa Antanarivo wakimshinikiza rais ajiuzulu.

Kulikuwepo na vitisho vya mapinduzi ya kijeshi iwapo serikali haingetekeleza amri ya mahakama ya katiba mwezi Mei iliyoagiza kutafuta mgombea wa muafaka wa nafasi ya waziri mkuu na kuunda serikali ya umoja wa kitaifa.

Kama waziri mkuu wa muafaka Christian Ntsay, mtaalamu wa shirikala Umoja wa Mataifa aliteuliwa kuwa waziri mkuu na sheria ya uchaguzi ikafanyiwa marekebisho.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *