Igp sirro afunguka kuhusu mo dewji; gari lahusiswa

Igp sirro afunguka kuhusu mo dewji; gari lahusiswa

Like
759
0
Friday, 19 October 2018
Local News

Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) Simon Sirro amesema polisi  wamepata maelezo muhimu kuhusu gari lililotumiwa na watu waliomteka mfanyabiashara Mo Dewji.

Amesema gari hilo lilitokea nchi jirani ambayo hakuitaja na kueleza kuwa liliingia nchini Tanzania mnamo 1 Septemba, amewaonesha wanahabari picha za gari hilo ambapo amesema wanaomba maelezo zaidi.

Kamanda Sirro amesema wanafuatilia kwa pamoja na polisi wa kimataifa wa Interpol.

Amesema kufikia sasa hawafahamu iwapo gari hilo bado lipo Tanzania na akawaomba wananchi kutoa taarifa kwa polisi wakiliona.

“Tumefuatilia na watu wetu wamekwenda mpaka mpakani na wameweza kuona lilipita 1 Septemba 2018. Tumepata maelezo ya kutosha ambayo siwezi kuyasema,” amesema.

Sirro amesema kwa kutumia kanda za kamera za CCTV wamebaini kwamba gari hilo aina ya Surf baada ya kutoka hoteli ya Colosseum, lilipita Hassan Mwinyi, mpaka maeneo mzunguko wa barabara ya kwenda Kawa.

 

“Bado watu wetu wanafuata kuonelea kama walielekea maeneo ya SilverSand au Kawa,” amesema.

“Hapo tunaamini gari hilo lilipotelea, tunakwenda jumba kwa jumba kutafuta.”

“Tumehakikisha pia kuna watu wetu watazunguka baadhi ya nchi hizo jirani.”

Kuhusu usaidizi kutoka nje, Kamanda Sirro amesema: “Tukiona kuna hiyo sababu tutamshauri Amiri jeshi Mkuu mheshimiwa Rais. kwa hali tuliyo nayo sidhani kama ipo sababu,” amesema Sirro.

Kamanda Sirro amepuuzilia mbali taarifa kwamba kuna uwezekano kamera za CCTV ‘zilichezewa’ na kwamba hazikuwa zinafanya kazi wakati wa tukio.

“Ile kanda haikuwa wazi sana kwa sababu ya wakati huo (asubuhi na mapema) na aliyekuwa anaifuatilia kwa wakati huo, lakini baadaye kwa kuunganisha maelezo mbalimbali, unaweza kupata maelezo,” amesema Sirro.

“Kama ilikuwa haifanyi kazi, hizo kanda ambazo hazikuwa wazi zilipatikana vipi?”

Watuhumiwa wanaoshikiliwa na polisi

Kamanda Sirro amesema kufikia sasa watu wanazuiliwa na polisi kuhusiana na kisa cha kutekwa kwa Mo.

Amesema watu wengine takriban 26 ambao walikuwa wanahojiwa wameachiliwa huru.

Mkuu huyo amesema kufikia sasa bado hawezi kubaini iwapo tajiri huyo aliyetekwa yuko hai au la.

Amewahimiza watu walio na uwezo wa kumiliki silaha kwa njia halali kufanya hivyo, na kusema ingawa taifa hilo ni salama ni vyema kuzingatia usalama wao.

Sirro amesema huenda Watanzania wasiwe hatari kwao lakini kukawa na watu wenye nia mbaya kutoka nchi nyingine.

Amewataka pia wananchi kutofautisha kati ya mtu kupotea na kutekwa.

Amesema wapo watu wanaotoroka makwao kwa hiari na kurejea baada ya miaka mingi.

“Nikitoka nikamwacha mke wangu nikaenda Marekani, mtasema IGP katekwa?” amesema.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *